Mwenyekiti wa chama cha Wiper Prof. Kivutha Kibwana amewatetea Wawakilishi Wadi wa Machakos kutokana na tetesi kwamba walikuwa na njama fiche ya kumhandaa Gavana Alfred Mutua kutia sahihi bajeti iliyo na dosari.Gavana Kibwana alisema kwamba bajeti hiyo iliwasilishwa na kupitishwa katika bunge la jimbo la Masaku na kwa kauli moja na watangulizi wao Juni mwaka jana.
Akiongea alipomtembelea mbunge wa Kathiani Hon. Robert Mbui huko Masaku hapo Jumapili ,Prof. Kibwana alisema kwamba Gavana Mutua alikuwa amekosea kwa kuwalaumu Wawakilishi Wadi kwa makosa ambayo hawakuyafanya.
“Hapa Machakos kuna shida kubwa sana na kama chama tutaketi pamoja na kufanya mazungumzo kutatua utata ulioko baina ya viongozi wetu”alisema Kibwana alipomtembelea Mheshiwa Robert Mbui ambaye aliumia baada ya vurugu kuzuka baina ya polisi na wafuasi wa upinzani wakati kiongozi wa NASA Mheshimiwa Raila Odinga alipowasili humu nchini kutoka ughaibuni mwezi jana.
Wiki jana Gavana Mutua alisema kuwa Wawakilishi Wadi walitaka kutumia sh.1.3 bilioni kwa kugharamia petroli kwa minajili ya usafiri wao na kudai pesa hizo zilitumika kufadhili miradi ya maendeleo.Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, ambaye alihutubia mkutano huo akiwa Ujerumani kwa runumu,aliwahimiza wafuasi wake wazidi kuunga mkono NASA.
“Mheshimiwa Mbui ni shujaa wenu ambaye aliumia akiwa katika harakati za kutetea maslahi yenu.Endeleeni kumuunga mkono na mzidi kukaa ndani ya muungano wa NASA.Safari ya kuenda Kanani bado ingalipo,”alisema Kalonzo Musyoka.